Na Gordon Kalulunga, Mbeya
MTOTO mchanga wa siku nne amefariki
dunia katika Hospitali teule ya wilaya ya Mbeya, Ifisi Mbalizi kwa kile mzazi
wake alichodai kuwa ni kutopata msaada kutoka kwa wauguzi wa Hospitali hiyo.
Tukio hilo limetokea usiku wa saa sita
Machi 27, mwaka huu ndani ya wodi ya wazazi hospitalini hapo.
Akizungumza na Gazeti hili nyumbani
kwao baada ya mazishi ya kichanga hicho, mama mzazi wa mtoto huyo Paulina Daud
(22), huku akilia alisema kuwa, alipelekwa Hospitalini hapo akiwa mjamzito
Machi 24, mwaka huu, majira ya saa tatu asubuhi ambapo saa tano alijifungua kwa
njia ya upasuaji.
“Mtoto alikuwa salama na alikuwa
akinyonya vizuri nami nikiwa naendelea kuuguza kidonda mpaka tarehe 26 usiku wa
saa nne mtoto akawa analia sana ndipo nikaomba msaada kwa muuguzi mmoja akasema
yeye hausiki na wodi letu” alisema Paulina.
Alisema pamoja na maumivu ya kidonda
chenye mshono, alipoona mtoto anazidi kulia akaamua kujikongoja mpaka chumba
cha wauguzi na kuwaeleza tatizo lake, badala ya kwenda kumsaidia wakamwambia
aende akamchukue mwanae na kumpeleka chumba walichokuwa wauguzi.
“Nikarudi wodini na kumbeba mtoto kwa
shida kisha kumpeleka chumba cha wauguzi na mmoja wa wauguzi akasema nimwamshe
mwenzake aliyekuwa amelala pembeni na nilipomwamsha wakamwangalia mwanangu
wakasema tayari amefariki” alisema Paulina huku akiangua kilio…
Mama mzazi wa Paulina Sekela Daud,
alisema kichanga tangu kipate uhai wake hakikuwa na matatizo yeyote na kwamba,
alipopata taarifa ya kifo hicho alishtuka na kuamua kutafuta usafiri kutoka
Mbalizi usiku huo na kwenda Hospitalini.
“Nilifika saa kumi na moja alfajiri
Hospitalini na niliwaomba walinzi waniruhusu kwa kuwaambia kuwa nilikuwa
nimeitwa na wauguzi kwa tatizo la mwanangu, wakaniruhusu na nilipofika nikakuta
hali hiyo na nilipowauliza wakasema hawajui sababu yeyote iliyosababisha kifo
cha mjukuu wangu” alisema Sekela.
Alisema baada ya taratibu na mabishano
kadhaa hospitalini hapo, wakaruhusiwa kutoka na maiti majira ya saa tatu
asubuhi na mama mzazi wa kichanga aliruhusiwa kutoka majira ya saa sita mchana
na anatakuwa kwenda Hospitalini hapo kutoa nyuzi April 5, mwaka huu.
Machi 29, mwaka huu, mwandishi wa
habari hii alifika katika Hospitali hiyo ya Ifisi Mbalizi na kufanya mahojiano
na Mganga mkuu mfawidhi wa hospitali hiyo Dr. Msafiri Kimaro, ambaye alisema
kuwa hakuwa na taarifa.
Baada ya mahojiano zaidi Dr. Kimaro
alimchukua mwandishi na kuongozana naye kwenda wodini kwa ajili ya kuangalia
nyaraka ambapo alijiridhisha kuwa mjamzito huyo alijifungua salama na mtoto
alikuwa salama lakini pia katika jarada la Paulina wataalam hao wameandika kuwa
hawajaona sababu yeyote iliyosababisha kifo cha mtoto huyo.
“Ninakuomba siku ya Alhamisi (Machi
31, mwaka huu), ufike kwa ajili ya taarifa zaidi ili nifuatilie” alisema Dr.
Kimaro.
Machi 31, mwaka huu, tayari timu ya
wataalam kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mbeya ilifika katika
hospitali hiyo kuhoji jambo hilo na mengine ambayo gazeti hili linaendelea
kujiridhisha likiwemo mwanamke aliyefanyiwa upasuaji na kushindwa kushonwa
vizuri na sasa tumbo lake limeanza kuvimba na anatakiwa kufanyiwa upasuaji mpya
ili ashone vyema katika hospitali ya wazazi Meta.
April mosi mwaka huu, mwandishi
alifika tena hospitalini hapo na kukutana na Mganga Mkuu wa Hospitali hiyo Dr.
Msafiri Kimaro na Katibu wa Hospitali hiyo, Dick Balagasi, ambapo walisema
maelezo yote mwandishi anapaswa kuyapata kwa wauguzi waliokuwa zamu maana wao
hawakuwepo siku tukio hilo likifanyika.
“Kalulunga lakini unapaswa kudumisha
mahusiano na nasi maana tumeambiwa kuwa unaishi jirani hapa, hivyo ni vema
tukadumisha mahusiano kuliko ukisikia jambo unaandika” alisema Balagasi kabla
hajakatishwa na kauli ya mwandishi wa habari kuwa “Hisia zisiondoe uhalisia”.
Hata hivyo ikumbukwe kuwa, mtindo wa
uongozi wa Hospitali hiyo kuwa na kifua kikubwa cha kuwatetea baadhi ya
watumishi wanaoshindwa kuwajibika vizuri ulisababisha mjamzito Sabina Mwakyusa
(28), kufukuzwa wodini na kujifungulia katika geti la hospitali hiyo kwa msaada
wa walinzi huku mvua ikinyesha usiku.
Tukio hilo lilitokea usiku wa Desemba 19, mwaka 2013,
ambapo baadhi ya wauguzi waliokuwepo katika chumba cha matazamio ya kujifungua,
walidaiwa kumfukuza na kumpiga mjamzito Sabina Mwakyusa(28) mkazi wa Kijiji cha
Iwala, kata ya Utengule Usongwe wilayani humo.
Sabina, alisema alifika hospitalini hapo Desemba 18, 2013 na alipimwa na
manesi ambapo walimwambia kuwa hawamuoni mtoto tumboni mwake.
‘’Baadaye akaja Daktari na kunipima, akaniambia mtoto anaonekana vizuri
na ningejifungua mtoto wa kike ndipo nikaendelea kusubiri uchungu zaidi’’
alisema Sabina.
Alisema ulipofika usiku wa Desemba 19 majira ya saa mbili usiku, alianza
kujisikia uchungu, ndipo manesi waliompima mwanzo wakamwambia anatakiwa apimwe
tena jambo ambalo alikataa kwa madai kuwa alikuwa akiumizwa, ndipo wakamwambia
aondoke hospitalini hapo kwasababu ana kiburi.
‘’Baada ya kuonekana mimi nasita kuondoka, wakaanza kunipiga na kunipatia
biki na kunilazimisha kuandika kuwa mimi sitaki kujifungulia hapo ndipo
tukatoka na mama na kwenda nje ya geti na kujifungulia getini huku mvua
ikinyesha’’alisema Sabina Mwakyusa.
Alisema, mama yake na baadhi ya wajawazito waliokuwepo ndani ya wodi
hilo, walijaribu kuwabembeleza wasimfukuze lakini walikataa.
Mama mzazi wa mwanamke huyo, Roda Mwakyusa(50), alisema anaumia
akikumbuka yaliyomkuta mwanaye ikiwa ni uzao wake wa kwanza.
‘’Niligaragara mweeeh! kuwaomba msamaha wale manesi ili wamsamehe na
kumhurumia huyu mtoto wangu, lakini walikataa wakisema kuwa ana kiburi sana’’
alisema Prisca Mwakyusa.
Alisema walipotoka wodini huku mwanaye uchungu ukimzidi, walifika getini
akazidiwa. Chupa ikapasuka. Damu zikaanza kumvuja; alikaa muda mrefu zaidi ya
saa moja na kuanza kujifungua ndipo walinzi wa kampuni ya Mult-Lion,
wakamsaidia kumpeleka katika upenu wa duka la hospitali hiyo ili kukwepa kokoto
zilizopo na mvua iliyokuwa ikinyesha.
Mkurugenzi wa kampuni ya ulinzi ya Mult-Lion, Kinanda Sanga, alipoulizwa
kuhusu tukio hilo, alisema kuwa hakuwa na taarifa lakini baada ya kuwauliza
askari wake walimpatia taarifa ya tukio hilo kuwa lilitokea na wao wakatoa
msaada.
Dada wa msichana huyo, Enitha Mwakyusa(35), alisema alipigiwa simu majira
ya saa tano usiku na mama yake mzazi akimweleza yaliyomkuta mdogo wake na
kwamba atafute gari la kwenda kuwachukua.
‘’Mama alinipigia simu usiku, nikawaamusha majirani ambao walikuwa na
namba za madereva tax, ambapo saa saba walifika hapa nyumbani Mapelele’’
alisema Enitha.
Wifi wa Sabina Mwakyusa, Prisca Nafred, alisema alimpeleka mtoto
aliyezaliwa katika hospitali hiyo majira ya saa saba mchana ya Desemba 20, kwa
ajili ya chanjo, lakini hakupata chanjo kwa madai kuwa alikuwa amechelewa
kufika, hivyo alitakiwa kufika siku ya Jumanne Desemba 24, mwaka huo.
Desemba 21, familia hiyo ilimpigia simu Mwandishi wa habari wakimweleza
kuhusu maendeleo mabaya ya mtoto ambapo Mwandishi wa habari hizi alimtaarifu
Mratibu wa afya ya mama na mtoto mkoa wa Mbeya, Prisca Butuyuyu, kuhusu suala
hilo ambapo makubaliano yaliafikiwa kuwa mtoto apelekwe Hospitali ya Rufaa,
kitengo cha wazazi Meta.
Mtoto huyo alipokelewa Meta na kuingizwa kwenye chumba cha joto kisha
kuanza kupatiwa matibabu kwa kuwekewa drip za maji mpaka Desemba 23 mwaka huu.
Mganga Mkuu wa wilaya ya Mbeya Louis Chomboko, alipopata taarifa,
alichukua hatua ya kwenda kumuona mtoto huyo katika hospitali ya Meta.
‘’Nimeonana na mama wa mtoto na kumuona mtoto chumba cha joto na kupata
maelezo yote ikiwa ni pamoja na maelezo ya file la Meta hivyo nipe nafasi tena
kufuatilia tukio hili hospitali ya Ifisi na tukibaini ukweli tutachukua hatua’’
alisema Dr, Chomboko akimsihi Mwandishi kutoandika kwanza habari hii.
Mwezi Desemba mwaka 2012, Mama mmoja(jina tunalo), aliyekuwa anaumwa BP,
alichomwa sindano (dawa)ambazo haziendani na ugonjwa wake na mmoja wa watoto
wake alipohoji kwa uongozi wa hospitali hiyo alijibiwa kuwa hapaswi kugombana
na wauguzi! Kisha akaitwa Dr. Kenneth, ambaye aliamua kuokoa maisha ya mama
huyo katika hospitali hiyo ya Ifisi kwa kumchoma sindano ya dawa iliyokuwa
ikitakiwa.
No comments:
Post a Comment