Monday 7 March 2016

Timu ya Taifa U21 ya Hockey yakabidhiwa bendera

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Nape Nnauye katika hafla ya kuiaga Timu ya Taifa ya Magongo U21 kwenda Windhoek, Namibia 
Timu ya Taifa ya Vijana chini ya miaka 21 (U21) ya mchezo wa magongo imetakiwa kupambana na kurejea na ushindi katika michuano ya vijana barani Afrika inayotarajia kuanza Machi 18 mwaka huu jijini Windhoek, Namibia.

Akizungumza katika hafla fupi ya kuikabidhi bendera timu hiyo jana, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Nape Nnauye ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana alisema ana imani kubwa kwa vijana hao ambao ni mara yao ya kwanza kufanya vizuri.

Nape alisisitiza, nidhamu watakayoionesha na kujituma katika michuano hiyo itakayotia nanga Machi 28 mwaka huu ikiwa ni sehemu ya kufuzu kucheza Kombe la Dunia la Vijana Novemba mwaka huu nchini India italitangaza taifa katika mchezo huo na utakuwa mwanzo mzuri.

Kwa upande wao manahodha wa timu hiyo Eliezer Jeremiah na Irene Albert walisisitiza kuwa licha ya kuwa ni mara yao ya kwanza kushiriki watajitahidi wawezavyo huku wakimsikiliza kocha wao ambaye amewapa mazoezi ya kutosha.

Kocha Valentine Quranta alisisitiza kuwa amekianda kikosi vizuri licha ya kwamba ushindani utakuwa mkubwa sana endapo atapangwa na Ghana, Kenya au Namibia ambao wako vizuri katika mchezo huo.

Pia Ofisa Mkuu wa Fedha wa NMB, Waziri Barnabas alisisitiza ulazima wa kuisaidia timu hiyo baada ya waziri kuwaomba wafadhili kujitahidi kuingia mikataba ya muda mrefu ili kuweka programu thabiti.

Aidha Mwenyekiti wa Chama cha Magongo Tanzania (THA), Ibrahim Sykes alisema wanaendelea na juhudi za kuupanua mchezo huo lakini wanakabiliwa na kikwazo cha vifaa suala kwa wizara husika.


Katika hafla hiyo, NMB walitoa shilingi mil. 25 na mabegi ya kusafiria huku Diamond Motors nao wakiunga mkono juhudi za timu hiyo.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye (katikati) akimkabidhi vifaa Mwenyekiti wa Chama cha Magongo Tanzania Abraham Sykes vilivyotolewa na NMB katika hafla ya kukabidhi bendera ya taifa kwa Timu ya Taifa ya Vijana ya Magongo U21  inayokwenda kushiriki Michuano ya Mataifa ya Afrika ya Vijana jijini Windhoek, Namibia. (Picha na Jabir Johnson)
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye (katikati) akiwa na manahodha wa Timu ya Taifa ya Vijana ya Magongo U21  Eliezer Jeremiah (wa pili kushoto) na Irene Albert (wa pili kulia), katika hafla ya kukabidhi bendera ya taifa kwa timu hiyo inayokwenda kushiriki Michuano ya Mataifa ya Afrika ya Vijana jijini Windhoek, Namibia.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye (kulia) akiwa na Katibu wa THA (kushoto), Mnonda Magani , Kocha Valentine Quranta (katikati) na viongozi wengine wa Timu ya Taifa ya Vijana ya Magongo U21  katika hafla ya kukabidhi bendera ya taifa kwa timu hiyo inayokwenda kushiriki Michuano ya Mataifa ya Afrika ya Vijana jijini Windhoek, Namibia.

No comments:

Post a Comment